Dkt. Akwilapo awataka wahitimu wa ADEM kusimamia kanuni na taratibu katika utendaji kazi.
    
   
  
 
 
 
 
  
  
  
  
  
  
    
  
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi 
na Teknolojia Dkt. Leornard Akwilapo amewataka wahitimu wa kozi za 
Uongozi na Usimamizi wa Elimu zinazotolewa na Wakala wa Maendeleo ya 
Uongozi wa Elimu (ADEM) kuhakikisha wanasimamia utekelezaji wa Sera ya 
Elimu na Mafunzo ya mwaka(2014), Sheria, Kanuni na Taratibu za Elimu ili
 kupunguza migogoro shuleni  
Katibu Mkuu ameyasema hayo katika 
mahafali ya Ishirini na tano (25) yaliyofanyika katika Chuo hicho 
kilichopo Bagamoyo Mkoani Pwani ambapo amewataka ADEM  kuendelea 
kusimamia utekelezaji wa Mtaala kwa ufanisi, kutoa takwimu sahihi za 
shule, kupanga mipango ya maendeleo ya shule inayotekelezeka, kusimamia 
fedha za elimu bila malipo kwa ufanisi.
Eneo lingine ambalo Katibu Mkuu ametaka 
litiliwe mkazo ni    pamoja na kudhibiti nidhamu za wanafunzi mara 
warudipo katika vituo vyao vya kazi.
Dkt. Akwilapo amesema mafunzo ya uongozi
 na usimamizi wa Elimu pamoja na Ukaguzi wa Shule ni muhimu katika 
kuwapa uwezo walimu na viongozi wa elimu kufanya kazi zao kwa weledi, 
ufanisi na kwa kujiamini zaidi hususani katika kipindi hiki cha 
maendeleo makubwa ya sayansi na teknolojia.
Amewataka wahitimu kuwa chachu ya 
mabadiliko katika Uongozi na Utawala Bora pamoja na  Uthibiti Ubora wa 
Shule nchini kwa kutumia ujuzi, maarifa, stadi na mbinu mpya 
walizozipata katika mafunzo ikiwa ni pamoja na   maarifa waliyoyapata 
kuyaeneza kwa walimu ambao hawajapata fursa ya kupata mafunzo hayo.
Source
WIZARA YA ELIMU,SAYANSI NA TEKNOLOJIA
24 November 2017 
Maoni